Kikosi cha kofia buluu cha Umoja wa Mataifa kikishirikiana na jeshi la serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo vinaendeleza operesheni za kijeshi dhidi ya waasi wa Uganda walioko katika jimbo la Orientale mashariki mwa Kongo.
Kanali Felix Prosper Basse Msemaji wa vikosi vya Umoja wa Mataifa nchini Kongo amesisitiza kuwa, operesheni hiyo inafanyika kwa lengo la kulisambaratisha kikamilifu kundi la waasi la Lord's Resistance Army LRA la nchini Uganda kwenye maeneo ya Haut na Bas – Uele katika jimbo hilo lililoko mashariki mwa Kongo.
Kanali Basse amesisitiza kuwa, vikosi vya Umoja wa Mataifa na vile vya jeshi la serikali ya Kinshasa kwa pamoja vina azma ya kukomesha kikamilifu vitisho vya waasi hao wa Uganda dhidi ya raia wa jimbo hilo. Kanali Basse amewataka waasi wa LRA kujisalimisha wenyewe kwa vikosi vya serikali na vile vya Umoja wa Mataifa. Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo licha ya kukabiliwa na harakati za waasi wa ndani, inakabiliwa pia na ukosefu wa usalama unaosababishwa na harakati za waasi wa Uganda na Rwanda ndani ya ardhi ya nchi hiyo
0 comments:
Chapisha Maoni